Tafuta

Papa:Usitazame maisha na wito kwa mtazamo wa ufanisi na matokeo ya haraka!

Katika ibada ya Misa ya iliyoongozwa na Papa katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro,Vatican kwa ajili ya kubariki mafuta ya Krisma,Papa emesema Bwana anawatafuta wanaoomboleza dhambi za Kanisa na dunia.Katika maisha ya kiroho,wale wasiolia hurudi nyuma.Kujuta ni dawa dhidi ya ugumu wa moyo na kujililia wenyewe haimaanishi kujihurumia na ameonya unafiki wa makleri,wale wanaotupatia baraka za zawadi ya machozi.Bwana haombi hukumu za dharau kwa wale wasioamini bali upendo na machozi.

Na Angella Rwezaula – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko ameongoza ibada ya Misa Takatifu katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, Siku ya Alhamisi Kuu tarehe 28 Machi 2024 kwa kusaidiana na Makamu, jimbo la Roma Kardina Angelo De Donatis, na kushiriki maelfu ya makuhani, wa Jimbo la Roma, mashemasi, Makardinali wa Curia Roma, wakuu wa Curia Romana na waamini wa Mungu. Katika Mahubiri yake marefu, ninaanza na kifungu cha hitimisho ambapo Papa Francisko alisema: "Asanteni wapendwa mapadre kwa mioyo yenu iliyo wazi na tulivu, asanteni kwa bidii na machozi yenu, asanteni kwa sababu mnaleta muujiza wa huruma ya Mungu kwa ndugu zetu katika dunia ya leo. Bwana awafariji awaimarishe na kukuthawabisha.  Katika mahubiri yake, kwa njia hiyo Baba  Mtakatifu alitafakari jinsi ambavyo Mtakatifu Petro, Mchungaji wa kwanza wa Kanisa letu katoliki alivyompoteza Kristo na kumkana mara tatu. Kwa majuto, Papa alikumbusha kuwa, macho ya Petro yalijaa machozi ambayo, yakiinuka kutoka katika moyo uliojeruhiwa, yalimkomboa kutokana na  mawazo yake ya uongo na kujihakikishia kwake. Kwani machozi hayo ya uchungu yalibadilisha maisha yake.”

Papa alisema: “Ndugu wapendwa mapadre, uponyaji wa moyo wa Petro, uponyaji wa Mtume, uponyaji wa mchungaji, ilikuja wakati, akiwa na huzuni na kutubu, alijiruhusu kusamehewa na Yesu. Uponyaji wake ulifanyika katikati ya machozi na kilio cha uchungu, ambacho kilisababisha upendo upya. Alhamisi hii kuu ya Mwaka wa Sala, Papa alipenda kushirikisha pamoja na mapadre wenzake mawazo juu ya kipengele cha maisha ya kiroho ambacho, alisema, kimepuuzwa kwa kiasi fulani, lakini bado ni muhimu. Papa alisema: “Hata neno nitakalotumia kwa kiasi fulani ni la kizamani, lakini linastahili kutafakariwa. Neno hilo ni majuto”. Kwa kuongeza Papa alisema kwamba neno kujuta linahusisha “kuchoma moyo” kwa uchungu na kuibua machozi ya toba, kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Petro kutostahili kwetu, bali kutoboa kwa manufaa kunakosafisha na kuponya moyo."

Misa ya Papa ya Kubariki Mafuta
Misa ya Papa ya Kubariki Mafuta

Papa alisema, "Mara tu tunapotambua dhambi zetu, mioyo yetu inaweza kufunguliwa kwa kazi ya Roho Mtakatifu, chanzo cha maji ya uzima ambayo hububujika ndani yetu na kuleta machozi machoni mwetu. Wale walio tayari kufichuliwa na kuacha macho ya Mungu yaingie mioyoni mwao, wanapokea zawadi ya machozi hayo, maji matakatifu zaidi baada ya yale ya ubatizo. "Hata hivyo, tunahitaji kuelewa waziwazi maana ya kujililia wenyewe. Haimaanishi kulia kwa kujihurumia, kama ambavyo mara nyingi tunajaribiwa kufanya. Kujililia sisi wenyewe, ina maana ya kutubu kwa dhati kwa ajili ya kumhuzunisha Mungu kwa dhambi zetu; tukitambua kwamba sisi daima tunabaki katika deni la Mungu, tukikiri kwamba tumepotoka kutoka katika njia ya utakatifu na uaminifu hadi kwenye upendo wa Yule aliyetoa uhai wake kwa ajili yake sisi."

Baba Mtakatifu akisisitiza amesema "Kupitia haya, inamaanisha kutazama ndani na kutubu juu ya kutokuwa na shukrani na kutokuwepo kwetu na kukiri kwa huzuni uwili wetu, ukosefu wa uaminifu na unafiki. Kwa kujielekeza macho yetu kwa mara nyingine tena kwa Bwana Msulibiwa na kujiruhusu tuguswe na upendo Wake, ambao daima husamehe na kuinua, kamwe haukatishi tamaa tumaini la wale wanaomtumaini Yeye", “alisema Papa Francisko. Kwa kuendelea alisema: "machozi yanayotiririka mashavuni mwetu, yanashuka ili kutakasa mioyo yetu, hata kama kulazimishwa kunahitaji juhudi, kunaleta amani. Sio, chanzo cha mahangaiko, bali ni uponyaji wa nafsi, kwa kuwa hutenda kama dawa ya kulainisha majeraha ya dhambi, na kututayarisha kupokea mapigo ya tabibu wa mbinguni, ambaye hugeuza miyo iliyovunjika; mioyo iliyotubu, mara  moja hulainishwa na machozi.” Alisisitiza Papa.

Misa ya ya kubariki Mafuta 28 Machi 2024
Misa ya ya kubariki Mafuta 28 Machi 2024

Baba Mtakatifu amekumbusha kwamba walimu wa maisha ya kiroho wanasisitiza juu ya umuhimu wa kuunganishwa, kama alivyokumbuka kwamba upyaji wote wa mambo ya ndani huzaliwa na kukutana kati ya huzuni yetu ya kibinadamu na huruma ya Mungu, na kuendeleza kwa umaskini wa roho, ambao unaruhusu utakatifu. Roho ututajirisha. “Ndugu mapadre tujitazame sisi wenyewe na kujiuliza ni sehemu gani dhamiri na machozi hucheza katika uchunguzi wetu wa dhamiri na sala zetu, na hasa ikiwa, kwa miaka inayopita, machozi yetu yanaongezeka." Alisisitiza Papa kwamba kadiri tunavyozidi kukua ndivyo tunavyolia kidogo, na badala yake tunaombwa tuwe kama watoto. Tukishindwa kulia," Baba Mtakatifu alionya, "tunarudi na kuzeeka ndani, ambapo wale ambao maombi yao yanakuwa rahisi na ya kina, yenye msingi wa kuabudu na kustaajabisha mbele za Mungu, hukua na kustaajabisha na  kukomaa. Wanapungua kujihusisha wenyewe na kushikamana zaidi na Kristo."

Papa aliendelea kujadili mshikamano kama kipengele kingine cha majuto. Moyo tulivu, uliokombolewa na roho ya Heri, unakuwa na mwelekeo wa kawaida wa kuzoea wengine. Badala ya kuhisi hasira na kashfa kwa makosa ya kaka na dada zetu, hulia dhambi zao. Papa aliwakumbusha waamini  kwamba Bwana, hutafuta zaidi ya yote katika wale waliowekwa wakfu kwake, wanaume kwa wanawake wanaoomboleza dhambi za Kanisa na za ulimwengu, na kuwa waombezi kwa niaba ya wote. "Ni mashuhuda wangapi ,mashujaa katika Kanisa wametuonesha njia hii! alitoa mshangao Papa Francisko: “Tunawafikiria watawa wa jangwani, Mashariki na Magharibi; maombezi ya mara kwa mara, katika kulia  machozi, ya Mtakatifu Gregory wa Narek; sadaka ya Wafransiskani kwa ajili ya Upendo usiopendekea; na wale mapadre wengi ambao, kama Yohane wa Ars, waliishi maisha ya toba kwa ajili ya wokovu wa wengine,” alikumbusha papa huku  akisema, “Huu si ushairi, bali ukuhani!

Siku ya Kikuhani Alhamisi Kuu
Siku ya Kikuhani Alhamisi Kuu

Papa aliwaambia makuhani jinsi ambavyo "Bwana anavyotamani kutoka kwao, wachungaji wake, sio ukali bali upendo, na machozi kwa wale ambao wamepotea." Ikiwa mioyo yao inahisi kuridhika, alisema, "msijibu kwa hukumu, lakini kwa uvumilivu na huruma. Tunahitaji kuwekwa huru kutokana na ukali na lawama, ubinafsi na tamaa, ukakamavu na kufadhaika, ili kujikabidhi kwa Mungu kikamilifu, na kupata ndani yake utulivu unaotukinga dhidi ya dhambi zetu, dhoruba zinatuzunguka pande zote!" Tuombe, na tutoe machozi kwa ajili ya wengine, kwa njia hii, tutaruhusu Bwana kufanya miujiza yake. Wala tusiogope, kwa kuwa hakika atatushangaza!

Papa ameeleza kuwa "Majuto siyo kazi yetu sana, bali ni neema ambayo, kwa hiyo, lazima itafutwe katika maombi." Akigeukia toba, ambayo aliiita zawadi kutoka kwa Mungu na kazi ya Roho Mtakatifu, Baba Mtakatifu alitoa mapendekezo mawili ya kukuza roho ya toba. Kwanza: ” Tuache kuangalia maisha yetu na wito wetu katika suala la ufanisi na matokeo ya haraka, na kushikwa na mahitaji na matarajio ya sasa; badala yake tuangalie mambo kinyume na upeo mkubwa wa wakati uliopita na ujao." Aliwahimiza mapadre na waamini wafikirie yaliyopita kwa kukumbuka uaminifu-mshikamanifu wa Mungu, kukumbuka msamaha Wake na kujikita imara katika upendo Wake,”na wakati ujao,“kwa kutazama lengo la milele ambalo tumeitiwa, ndilo kusudi kuu la maisha yetu.  Kupanua upeo wetu, husaidia kupanua mioyo yetu, kutumia wakati na Bwana na kupata uzoefu.

Mafuta matakatifu
Mafuta matakatifu

Pili, Baba Mtakatifu alitoa wito kwa "mapadre kugundua tena haja ya kukuza binafasi ambayo si ya lazima na ya kazi, lakini iliyochaguliwa kwa uhuru, utulivu na wa muda mrefu. Turudi kwenye ibada na sala ya moyo. Papa aliendelea kuwaalika mapdre kurudia, 'Yesu, Mwana wa Mungu, unihurumie mimi mwenye dhambi.' Tuone ukuu wa Mungu hata tunapotafakari juu ya dhambi zetu wenyewe, na kufungua mioyo yetu kwa nguvu ya uponyaji ya macho yake, Papa alishauri kwamba hii itawawezesha makleri kugundua tena hekima ya Mama Mtakatifu wa Kanisa kwa kuanza maombi yetu  kwa maneno ya maskini aliaye: Ee Mungu, nisaidie!

Akirejea kwa Mtakatifu Petro na machozi yake, Baba Mtakatifu alisema kwamba: “Altare tunayoiona juu ya kaburi lake inatufanya tufikirie nyakati zote ambazo sisi makuhani  ambao kila siku husema: ‘Chukueni hiki nyote, mle kwa ajili yake ni Mwili wangu, ambao utatolewa kwa ajili yenu'. Tumemkatisha tamaa na kumhuzunisha Yule ambaye alitupenda sana kiasi cha kuifanya mikono yetu kuwa vyombo vya uwepo Wake. Tunafanye  vizuri, kurudia sala hizo tunazosema kimya: 'Kwa roho ya unyenyekevu na moyo uliopondeka na tukubaliwe nawe, Bwana, na unioshe, ee Bwana, na uovu wangu. na kunitakasa na dhambi yangu. Moyo wa mtu ukivunjika, hakika Yesu anaweza kuufunga na kuuponya." Kwa njia hiyo Papa alitoa shukrani kwamba: "Asanteni, mapadre wapendwa, kwa mioyo yenu iliyo wazi na tulivu... bidii yenu yote na machozi yenu, na kwa sababu mnaleta muujiza wa huruma ya Mungu kwa kaka na dada zetu katika ulimwengu wa leo. " Baba Mtakatifu Francisko alihitimisha kwa kusali kwamba Bwana "awafariji, awaimarishe na kuwatuza mapadre wake waaminifu."

Mahubiri ya Papa 28 Machi siku ya Alhamisi Kuu misa ya Krisma

Ndugu msomaji yafuatayo ni mahubiri kamili ya Baba Mtakatifu Francisko tarehe 28 Machi 2024

Katika mahubiri yake Baba Mtakatifu ameanza kusema kuwa “Katika sinagogi watu wote walimkazia macho” (Lk 4,20). Kifungu hiki cha Injili daima kinashangaza, ambacho kinatuongoza kuibua tukio hilo: kufikiria wakati ule wa ukimya ambapo macho yote yalielekezwa kwa Yesu, katika mchanganyiko wa ajabu na kutoaminiana. Hata hivyo, tunajua jinsi ilivyoisha: baada ya Yesu kufichua matarajio ya uwongo ya wanakijiji wenzake, “walijawa na ghadhabu”(Lk 4:28 ), wakatoka na kumfukuza nje ya jiji. Macho yao yalikuwa yamemkazia Yesu, lakini mioyo yao haikuwa tayari kubadili neno lake. Hivyo walikosa fursa ya maisha. Kwa njia hiyo Baba Mtakatifu amesema kuwa katika siku ya Alhamisi Kuu, ubadilishanaji mbadala wa kutazama hunafanyika. Mhusika mkuu ni Mchungaji wa kwanza wa Kanisa letu, Petro. Hapo mwanzo yeye pia hakuliamini neno la “kufichua” ambalo Bwana alikuwa amemwambia: “Utanikana mara tatu” (Mk 14:30). Kwa hiyo, ‘alimpoteza’ Yesu na kumkana wakati jogoo anapowika. Lakini basi, “Bwana alipogeuka na kumkazia macho”, “akakumbuka neno lile aliloambiwa na Bwana [...] Akatoka nje akalia kwa uchungu” (Lk 22,61-62). Macho yake yalibubujikwa na machozi ambayo, yakitiririka kutoka moyo uliojeruhiwa, yalimkomboa kutoka katika imani potofu na uhalali. Kilio hicho cha uchungu kilibadili maisha yake. Kwa miaka mingi, maneno na ishara za Yesu hazikuwa zimemsukuma Petro kutoka kwa matarajio yake, sawa na yale ya watu wa Nazareti: yeye pia alikuwa akimngojea Masiha wa kisiasa na mwenye nguvu, mwenye uwezo na mwenye maamuzi, na kukabili kashfa ya Yesu dhaifu, alikamatwa bila upinzani wa kupinga, alitangaza: “Simjui” ( Lk 22:57 ).

Na ni kweli, hakumjua: alianza kumjua wakati, katika giza la kukataa, alifanya nafasi ya machozi ya aibu, machozi ya toba. Naye atamjua kweli wakati, “alipoumia hata akamwuliza kwa mara ya tatu: “Je, wanipenda?”, anajiruhusu kupenywa kikamilifu na macho ya Yesu.” Kisha kutokana na “ Simjui” ataendelea kusema: “Bwana, wewe wajua yote” (Yh 21:17). Baba Mtakatifu amewaeleza makuhani, kuwa uponyaji wa moyo ya  Petro, uponyaji wa Mtume, uponyaji wa Mchungaji hutokea wakati, tukiwa na majeraha na kutubu, tunajiruhusu kusamehewa na Yesu: unapitia machozi, machozi ya uchungu, maumivu ambayo yanaturuhusu kugundua tena mapenzi. Baba Mtakatifu  amesema kuwa ndiyo sababu alihisi kuwa anapaswa kushirikisha nao  baadhi ya mawazo juu ya kipengele ambacho kimepuuzwa lakini ni muhimu cha maisha ya kiroho; Kwa hiyo amekipendekeza tena leo hii kwa neno ambalo labda limepitwa na wakati, lakini ambalo Papa anamini litatusaidia kugundua tena, neno lenyewe ni kujuta. Neno hilo huibua kuchomwa: majuto ni kuchomwa kwa moyo, kutobolewa kunakomtia majeraha, na kusababisha machozi ya toba kutiririka. Kipindi, ambacho kinamhusu Mtakatifu Petro tena, kinatusaidia. Yeye, akiwa ametiwa moyo na macho na maneno ya Yesu mfufuka, siku ya Pentekoste, akiwa ametakaswa na kuwashwa na Roho, alitangaza kwa wakazi wa Yerusalemu: “Mungu alimfanya huyu Yesu ambaye ninyi mlimsulubisha kuwa Bwana na Kristo” (rej. Mdo 2:36). Wasikilizaji walihisi maovu waliyokuwa wamefanya na wokovu ambao Bwana alikuwa akiwapatia, na “waliposikia mambo haya - linasema andiko - walihisi mioyo yao ikichomwa.”  (Mdo 2:37).

Hapa kuna utii: sio hisia ya hatia ambayo inakuangusha chini, sio ujanja ambao hupooza, lakini ni uchungu wa faida ambao huwaka ndani na huponya, kwa sababu moyo, unapoona ubaya wake na kujitambua kama mwenye dhambi unafungua, unakaribisha utendaji wa Roho Mtakatifu, maji yaliyo hai ambayo huisukuma, na kufanya machozi yatiririke usoni mwake. Yeyote anayetupa barakoa na kumwacha Mungu atazame moyoni mwake anapokea zawadi ya machozi haya, maji matakatifu zaidi baada ya yale ya Ubatizo.  Baba Mtakatifu amewasisitizia wapendwa mapadre kwamba “leo ninawatakia haya!” Hata hivyo, akielendelea alisema kuwa tunahitaji kuelewa vizuri maana ya kujililia wenyewe. Haimaanishi kujihurumia, kama vile mara nyingi tunashawishiwa kufanya. Hilo hutukia, kwa mfano, tunapokatishwa tamaa au kuhangaishwa na matarajio yetu yasiyofanikiwa, kuhusu ukosefu wa uelewaji wa wengine, labda ndugu na wakubwa wetu. Au wakati, kwa furaha ya ajabu na isiyo ya afya ya nafsi, tunapenda kukaa juu ya makosa ambayo tumepokea ili kujihurumia, tukifikiri kwamba hatujapata kile tulichostahili na kufikiria kwamba wakati ujao tunaweza tu kutuhifadhi mshangao mbaya unaoendelea.  Katika hili  Mtakatifu Paulo anatufundisha  kuwa  ni huzuni kulingana na ulimwengu, kinyume na huzuni kwa mujibu wa Mungu. Kujililia sisi wenyewe, hata hivyo, ni kutubu kwa dhati kwa kumhuzunisha Mungu kwa dhambi; ni kutambua kwamba sisi daima tuko katika madeni na kamwe katika mikopo; ni kukubali kwamba tumepoteza njia ya utakatifu, bila kuweka imani katika upendo wa Yeye ambaye alitoa maisha yake kwa ajili yetu. “Ni kuangalia ndani yangu na kulalamika juu ya kutokuwa na shukrani kwangu na kutokuwa na msimamo wangu; ni kutafakari kwa huzuni juu ya uwili na uwongo wangu; ni kushuka ndani ya kina cha unafiki wangu,, Papa ameongeza kusema “unafiki wa makasisi, ndugu wapendwa, unafiki huo ambao tunateleza sana, sana ... Jihadharini na unafiki wa makleri.”

Misa katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro
Misa katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro

Na hili basi kuinua macho yangu kwa Msalabani na kujiruhusu nisukumwe na upendo wake ambao daima husamehe na kuinua, ambao hauachi kamwe matarajio ya wale wanaomtumaini Yeye kukatishwa tamaa. Hivyo machozi yanaendelea kumwagika na kutakasa moyo. Kuunganisha, kiukweli, kunahitaji juhudi lakini hurejesha amani; hauleti uchungu, bali huifanya roho iwe nyepesi kutoka kwa mizigo, kwa sababu inatenda katika jeraha la dhambi, ikitutayarisha kupokea papo hapo kubembelezwa na Bwana ambaye anabadilisha moyo wakati “umetubu na kuvunjika” (Zab 51:19),kulainishwa na machozi. Kwa hiyo kushikana ni dawa ya (sclerocardia), ugumu wa moyo ulioshutumiwa sana na Yesu (rej. Mk 3:5; 10:5). Moyo, kiukweli, bila toba na machozi, huwa mgumu: kwanza unakuwa wa mazoea, kisha usiyestahimili shida na kutojali watu, kisha baridi na usiwe na hisia, kana kwamba umefungwa kwenye ganda lisiloweza kuvunjika, na mwishowe unakuwa moyo wa jiwe. Lakini, kama tone linavyochimba jiwe, ndivyo machozi yanavyochimba polepole mioyo migumu. Hivyo tunashuhudia muujiza wa huzuni, wa huzuni nzuri ambao unaongoza kwa utamu. Kwa njia hiyo baadaye tunaelewa kwa nini walimu wa kiroho wanasisitiza juu ya majuto. Mtakatifu Benedikto anatualika kila siku “kukiri kwa Mungu kwa machozi na kulilia  dhambi zetu za zamani”, na anasema kwamba kwa kuomba “hatutasikilizwa kwa maneno yetu, bali kwa usafi wa moyo na kwa maelewano ambayo hutupatia machozi.”Na ikiwa kwa Mtakatifu Yohane Chrysostom chozi moja huzima moto wa dhambi, Mwiga wa Kristo anapendekeza: “Jiachilie chini ya utii wa moyo, kwa sababu ya wepesi wa moyo na kutojali kwa kasoro zetu mara nyingi hatutambui matatizo ya nafsi zetu.” Majuto ni dawa,, kwa sababu kunaturudisha kwenye ukweli wetu wenyewe, ili kwamba kina cha kuwa kujielewa kwetu kuwa wenye dhambi kinadhihirisha ukweli mkuu zaidi wa kusamehewa kwetu na  furaha ya kusamehewa.

Kwa hiyo kauli ya Isaka wa Ninawi haishangazi anaposema: “Mwenye kusahau kipimo cha dhambi zake mwenyewe husahau kipimo cha neema ya Mungu kwake”. Ni kweli, Papa Francisko amesisitiza kuwa, kila kuzaliwa upya ndani yetu siku zote hutokana na kukutana kati ya taabu zetu na huruma zake – “taabu zetu na huruma zake zikutane -, kila kuzaliwa upya ndani” hupitia umaskini wetu wa roho ambayo unaruhusu Roho Mtakatifu kututajirisha. Kauli za nguvu za walimu wengi wa kiroho zinaweza kueleweka katika nuru hii. Hebu tufikirie maneno ya kutatanisha ya Mtakatifu Isaka: “Yeye anayejua dhambi zake mwenyewe [...] ni mkuu kuliko yeye ambaye huwafufua wafu kwa njia ya maombi. Anayejililia kwa saa moja ni mkuu kuliko anayetumikia ulimwengu wote kwa kutafakari [...]. Aliyepewa kujijua mwenyewe ni mkuu kuliko yeye aliyepewa kuona malaika.” Baba Mtakatifu akiendelea amerudi kwao, mapadre, na kwamba “tujiulize ni kiasi gani cha matusi na machozi yapo katika uchunguzi wetu wa dhamiri na katika maombi yetu. Tujiulize kama miaka inavyosonga machozi yanaongezeka. Kwa mtazamo huo ni vizuri kwamba kinyume chake hutokea ikilinganishwa na maisha ya kibaolojia, ambapo, unapokua, hulia kidogo kuliko wakati ukiwa mtoto.

Siku ya Kikuhani
Siku ya Kikuhani

Katika maisha ya kiroho, hata hivyo, ambapo kuwa watoto huhesabika (rej. Mt 18:3), wale ambao hawalii wanazeeka ndani, wakati wale wanaofikia sala rahisi na ya ndani zaidi, iliyofanywa kwa kuabudu na hisia mbele za Mungu, wanakomaa.”Anajifunga mwenyewe kidogo na kidogo kwake na zaidi kwa Kristo, na anakuwa maskini wa roho. Kwa njia hii anahisi kuwa karibu na maskini, mpendwa wa Mungu, ambaye hapo awali - kama Mtakatifu Francis anaandika katika mapenzi yake - alijitenga kwa sababu alikuwa katika dhambi, lakini ushirika wao unatoka katika uchungu hadi utamu. Na kwa hivyo yule anayeomboleza moyoni mwake kila wakati hujihisi zaidi kama ndugu kwa wakosefu wote ulimwenguni, anahisi zaidi kama ndugu, bila mfano wa ubora au ukali wa hukumu, lakini kila wakati kwa hamu ya kupenda na kurekebisha. Na hiyo ni tabia nyingine ya majuto ambayo ni mshikamano. Moyo mtulivu, uliomulikwa  kwa roho ya Heri, unakuwa na mwelekeo wa kawaida wa kuwa na masikitiko kwa ajili ya wengine: badala ya kukasirika na kuchukizwa na uovu unaofanywa na ndugu, hulia kwa ajili ya dhambi zao. Haukuashifu! Papa ameongeza kusema kuwa aina fulani ya mabadiliko hutokea, ambapo mwelekeo wa asili wa kujifurahisha mwenyewe na kutobadilika na wengine hubatilishwa na, kwa neema ya Mungu, mtu anakuwa thabiti kwake mwenyewe na kuwahurumia wengine.

Na Bwana anawatafuta, hasa miongoni mwa wale waliowekwa wakfu kwake, wale wanaoomboleza dhambi za Kanisa na za ulimwengu, kuwa chombo cha maombezi kwa ajili ya wote. Ni mashahidi wangapi mashujaa katika Kanisa wanaotuonesha njia hii! Hebu tuwafikirie watawa wa jangwani, Mashariki na Magharibi; kwa maombezi yenye kuendelea, yanayojumuisha kulia na machozi, ya Mtakatifu Gregory wa Narek; kwa sadaka ya Wafransiskani kwa Upendo usiopendwa; kwa makuhani, kama Tiba ya Mtakatifu wa  Ars, aliyeishi kwa toba kwa ajili ya wokovu wa wengine Papa amehimiza, kuwa huu sio ushairi, huu ni ukuhani! Papa kwa kuongeze “zaidi kutoka kwetu sisi Wachungaji wake, Bwana haombi hukumu za dharau kwa wale wasioamini, bali upendo na machozi kwa wale walio mbali. Hali ngumu tunazoona na uzoefu, ukosefu wa imani, mateso tunayogusa, katika kuwasiliana na moyo uliovunjika haichochei uthabiti katika mabishano, lakini uvumilivu katika huruma.”

Misa katika kanisa Kuu la Mtakatifu  Petro
Misa katika kanisa Kuu la Mtakatifu Petro

Ni jinsi tunavyohitaji kuwa huru kutokana na ukali na kashfa, kutoka ubinafsi na tamaa, kutoka katika ukaidi na kutoridhika, kumwamini na kujikabidhi kwa Mungu, kutafuta ndani yake amani ambayo inaokoa kutoka katika kila dhoruba! Tunaabudu, kuombea na kulia kwa ajili ya wengine: tutamruhusu Bwana kufanya maajabu. Na tusiogope: atatushangaza! Huduma yetu itafaidika nayo.” Papa amewasahuri Makuhani. Leo, katika jamii ya kiulimwengu, tuna hatari ya kuwa watendaji sana na wakati huo huo kuhisi kutokuwa na nguvu, na matokeo ya kupoteza shauku na kujaribiwa kuvuta makasia, kujifunga wenyewe kwa malalamiko  lakini ole wao wa  malalamiko - na kuufanya ukuu wa matatizo kushinda ukuu wa Mungu.” Papa Francisko ameonya. Hili likitokea, tunakuwa na uchungu na kuumwa, kila mara tukisema vibaya, kila mara tunapata fursa ya kulalamika. Lakini ikiwa badala yake uchungu na majuto hayaelekei ulimwengu, bali kwa moyo wa mtu mwenyewe, Bwana hakosi kututembelea na kutuinua. Kama vile Kumwiga Kristo hutuhimiza kufanya: “Usichukue mambo ya watu wengine ndani yako, hata usijisumbue na yale ambayo watu mashuhuri hufanya; badala yake daima jiangalie mwenyewe kwanza kabisa, na ushughulikie onyo lako hasa kwako mwenyewe, kabla ya watu wengine, hata kwa wapendwa.” Papa amesisitiza kuwa: “Husihuzunike ikiwa hupati upendeleo wa watu; kinachopaswa kukuelemea na kukuhuzunisha, hata hivyo, ni kutambua kwamba hauko kabisa na hakika kwenye njia ya wema.

Hatimaye, Papa alipenda kusisitiza kipengele muhimu: majuti  sio matunda ya zoezi letu, lakini ni neema na hivyo lazima iombwe katika sala. Toba ni zawadi kutoka kwa Mungu, ni tunda la utendaji wa Roho Mtakatifu. Ili kuwezesha ukuaji wake, Papa emeshirikisha vidokezo viwili vidogo. Cha kwanza sio kutazama maisha na wito kutoka katika mtazamo wa ufanisi na upesi, unaohusishwa tu na leo na uharaka na matarajio yake, lakini kwa siku za nyuma na zijazo kwa ujumla. Papa me kuwa zamani, kwa kukumbuka uaminifu wa Mungu – Mungu ni mwaminifu, akikumbuka msamaha wake, akitutia nanga katika upendo wake; na ya wakati ujao, tukifikiria lengo la milele ambalo tumeitiwa, lengo kuu la kuwepo kwetu. Kwa hiyo, “kupanua upeo wako husaidia kupanua moyo wako, kukuchochea kurudi kwako mwenyewe na Bwana na kuishi kwa utulivu. Ushauri wa pili, ambao Papa amedokeza kuwa unakuja kama matokeo ni kwamba  bora tugundue tena hitaji la kujitolea kwa sala isiyostahili na inayofanya kazi, lakini ya bure, tulivu na ya muda mrefu. Swali:  je, maombi yako yakoje? Hurudi kwenye ibada - umesahau kuabudu? - na turudi kwenye maombi ya moyo. Turudie kusema: Yesu, Mwana wa Mungu, nihurumie mimi mwenye dhambi. Tutahisi ukuu wa Mungu katika unyenyekevu wetu kama wenye dhambi, kutazama ndani yetu na kuruhusu macho yake kupita ndani yetu. Tutagundua tena hekima ya Mama Mtakatifu wa Kanisa, ambayo daima hututambulisha kwa sala kwa wito wa maskini wanaolia: "Ee Mungu, njoo uniokoe."

Alhamisi Kuu
Alhamisi Kuu

Papa Francisko akiendelea na mahubiri hayo alisema “hatimaye turudi kwa Mtakatifu Petro na machozi yake. Altare iliyowekwa juu ya kaburi lake haiwezi isitusaidia kufikiria ni mara ngapi sisi, tunaosema pale kila siku kwamba: “Chukueni nyote mle: huu ndio Mwili wangu unaotolewa sadaka kwa ajili yenu, ni mara ngapi tunamkatisha tamaa na kumhuzunisha Yeye ambaye anatupenda hadi kufikia hatua ya kuifanya mikono yetu kuwa vyombo vya uwepo wake. Kwa hiyo ni vyema kuyafanya maneno hayo kuwa yetu  ambayo tunajitayarisha kwayo kwa kunong’ona: “Wanyenyekevu na wenye kutubu, utukaribishe, ee Bwana”, na tena: “Ee Bwana, unioshe na hatia yangu, unifanye safi kutoka  dhambi yangu.” Katika yote, tunafarijiwa na uhakika tunaopewa leo hii kwa Neno: Bwana, aliyewekwa wakfu kwa upako ( Lk 4:18),amekuja kufunga jeraha za mioyo iliyovunjika” (Is 61). 1). Kwa hiyo, moyo ukipasuka unaweza kufungwa na kuponywa na Yesu.  Papa amewashukuru mapadre kwamba “Asante, wapendwa mapadre, asante kwa mioyo yenu iliyo wazi na tulivu; asante kwa kazi yenu na asante kwa machozi yenu; asante kwa sababu mnaleta ajabu ya huruma - kusamehe daima, kuwa na huruma - na kuleta huruma hii kwa Mungu kwa kaka  na dada wa wakati wetu. Wapendwa makuhani, Bwana na awafariji, awathibitishie na kuwathawabisha. Asante.” Amehimitisha.

28 March 2024, 12:33