Tafuta

2023.08.13  Wakati wa sala ya Malaika wa Bwana, Uwanja wa Mtakatifu Petro ulijaa vijana walioshiriki siku ya vijana duniani huko Lisbon ambao Papa amewasalimia. 2023.08.13 Wakati wa sala ya Malaika wa Bwana, Uwanja wa Mtakatifu Petro ulijaa vijana walioshiriki siku ya vijana duniani huko Lisbon ambao Papa amewasalimia. 

Maombi ya Papa kwa ajili ya Cameroon na salamu kwa vijana wa WYD

Akishangiliwa kwa nderemo na vifijo mwishoni mwa Sala ya Malaika wa Bwana,Papa Francis amesalimia baadhi ya makundi ya vijana walioshiriki katika Siku ya Vijana Duniani huko mjini Lisbon.Ametoa hata wito wa amani kwa ajili ya nchini Cameroon, iliyokumbwa na ghasia na vita.

Na Angella Rwezaula, - Vatican.

Akiwa katika  dirisha la Jumba la Kitume, mara baada ya sala ya Malaika Dominika tarehe 13 Agosti 2023, Baba Mtakatifu ameomba sala kwa ajili ya amani nchini Cameroon ambapo tarehe 14 Agosti ni  mkesha wa sikukuu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni, watafanya  hija katika jimbo la Bafoussam ili kuombea amani nchini humo ambayo bado inakumbwa na ghasia na vita. Kwa njia hiyo Baba Mtakatifu amesema: “Kesho, katika mkesha wa sikukuu ya Mama Yetu Mpalizwa Mbinguni, ifafanyika hija ya kuomba amani nchini, ambayo bado inakumbwa na ghasia na vita, huko Bafoussam, Cameroon. Tuungane katika sala ya pamoja na ndugu zetu wa Cameroon ili kwa maombezi ya Bikira, Mungu aweze kudumisha tumaini la watu ambao wamekuwa wakiteseka kwa miaka mingi, na kufungua njia za mazungumzo ili kufikia maelewano na amani.”

Vita vya wenyewe kwa wenyewe  2017

Nchini Cameroon, vita vya wenyewe kwa wenyewe vimekuwa vikiendelea tangu 2017, ambavyo vilianza kutokana na migogoro ya kijamii na kiutamaduni. Pia inajulikana kama mgogoro au mzozo huo ulitokana na uasi uliofanywa na watu wanaozungumza Kiingereza wanaotaka kujitenga dhidi ya vikosi vya kawaida vya jeshi. Katika kukabiliana na hali hiyo, serikali ilituma jeshi katika mikoa inayozungumza Kiingereza ili kukabiliana na wapinzani. Katika miezi sita ya kwanza , ya mwaka  2023, vurugu na ukandamizaji vimeongezeka. Huku nyuma, misukosuko ya kisiasa iliyohusishwa na mrithi wa Rais Paul Biya mwenye umri wa miaka 90, ambaye ameongoza tangu 1982.

Kuombea Ukraine

Katika muktadha wa mgogoro huo wazo la Baba Mtakatifu  Francisko kama kawaidia yake limegeukia kwa mara nyingine  tena “kwa nchi ya Ukraine inayoteswa sana na vita”.

Bendera za vijana wa WYD

Papa Francisko akitazama katika uwanja uliojaa bendera nyingi kutoka sehemu mbali mbali za mataifa, amesema: “Sasa ninatoa salamu zangu kwenu nyote, Warumi na mahujaji kutoka nchi mbalimbali. Ninasalimia hasa baadhi ya vikundi vilivyoshiriki katika Siku ya Vijana huko Lisbon… Ni wengi! Ninaona bendera… Poland, Mexico, Argentina, Italia, Salvador, nyingi! Mapadre na vijana wa El Salvador ambao wana nguvu sana; wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Ibero-Amerika cha Puebla, Mexico; na vijana wa Taiwan. Tembeeni  vizuri! Na ninawatakia Dominika  njema. Tafadhali msisahau kuniombea. Mlo mwema,  mchana mwema na kwaheri ya kuonana!

tarehe 13 Agosti Papa ameomba
13 August 2023, 13:51