Tafuta

2023.07.12 NI WASHIRIKI WA WARSHA YA SIGNIS AFRIKA INAYOFANYIKA HUKO KAMPALA UGANDA KUHUSU MADA YA UHAMIAJI NA UKIMBIZI 2023.07.12 NI WASHIRIKI WA WARSHA YA SIGNIS AFRIKA INAYOFANYIKA HUKO KAMPALA UGANDA KUHUSU MADA YA UHAMIAJI NA UKIMBIZI 

Kard.Czerny,Signis Afrika:maoni ya Papa Francisko kwa wahamiaji na wakimbizi

Katika Warsha ya Waandishi wa Habari wa Kikatoliki kuhusu 'kuripoti masuala ya wahamiaji na wakimbizi,'Kardinali Czerny alituma ujumbe wake ukiongozwa na mada:“Maono ya Papa Francisko kuhusu wahamiaji na wakimbizi:Mafunzo kwa wafanyakazi wa vyombo vya habari katoliki”.Warsha ilianza tarehe 11 -16 Julai 203 huko Kampala.

Na Angella Rwezaula, - Vatican

Rais wa Baraza la Kipapa la Huduma ya Maendeleo ya Binadamu, Michael Czerny S.J. alituma ujumbe wake wakati wa ufunguzi wa Warsha ambao uliosomwa na mwakilishi wa Baraza hilo Dk. Mercedes De La Torre kwa wawakilishi wa Warsha kuhusu Uhamiaji wa Ukimbizi, iliyoandaliwa na SIGNIS Afrika huko Kampala Uganda ukianza  kutoa shukrani ya kumwalika  kushirikisha baadhi ya maneno ya utangulizi katika warsha yao. Kwa maana hiyo katika hotuba yake alianza kutoa maswali kwa ajili ya tafakari yao, kulingana na mafundisho ya Papa Francisko, na kuoneshe baadhi ya nyaraka ambazo wanaweza kupata msaada kwa kazi yao. Katika ujumbe wake wa Siku ya 109 ya Wahamiaji na Wakimbizi Duniani 2023, ambayo itafanyika tarehe 24 Septemba 2023, Papa Francis alichagua kauli mbiu ya  'Huru wa kuchagua kama Kuhama au Kukaa'. Je, hii ina maana gani kwa waandishi wa habari barani Afrika? “Kwanza, kama Kanisa la Kisinodi lililoalikwa kutembea karibu na wahamiaji na wakimbizi, ujumbe wa mwaka huu unafafanua kile mnachopaswa kufanya.

Waandishi wa habari wana jukumu la kutoa simulizi mpya, kuwaweka ndugu zetu wahamiaji, pamoja na familia zao, katikati, wakiunganisha mateso na matarajio yao na sababu za uhamiaji wao na kujua ni kwa nini nyuma ya kulazimishwa kwao kukimbia ili kuungana na suluhisho ambazo zingemaliza au kuponya uhamishaji wao.” Njaa; migogoro mipya na ya muda mrefu; mateso; majanga ya asili, vita; na mengine ambayo hufanya isiwezekane kuendelea kuishi maisha ya heshima na yanayoendelea katika nchi ya mtu. Mambo kama haya yanawalazimu takriban wakimbizi milioni 35 kuyaacha makazi yao, kuvuka mipaka ya kimataifa, pamoja na, mara mbili ya watu milioni 71 waliokimbia makazi yao ndani. Ikiwa tunasikiliza kwa makini kila mhamiaji au mkimbizi au mtu aliyehamishwa, tunagundua kwamba tamaa yao kuu ni kurudi mahali pao na kuishi kwa adabu na usalama. Lakini hadi sababu zinazowalazimisha kukimbia zipatiwe ufumbuzi, hakuna suluhisho linalowezekana.

Kwa wazi jukumu kuu ni la nchi asilia na viongozi wao, ambao wameitwa kufanya siasa nzuri  ambayo ni ya uwazi, uaminifu, mtazamo wa mbali na huduma ya wote, hasa wale walio hatarini zaidi,”anabainisha katika ujumbe wake. “Ni muhimu kuwasikiliza ndugu zetu tunaposonga kwani wanapaswa kuwa wahusika wakuu wa suluhisho za amani na maendeleo katika nchi zao. Waache waeleze matarajio yao. “Kwa maana hiyo Kardinali Cerni anawahasa waandishi wa habari,  ambao anasema wako katika nafasi nzuri ya kusikiliza kilio chao na kutangaza matarajio yao kwa ulimwengu. Kwa hivyo, wanakuwa wachangiaji wa mazoezi ya siasa nzuri, kuziba matamanio ya wahamiaji na kutoa mapendekezo kuelekea suluhisho linalowezekana kwa shida zao. Kwa kukuza haki ya kubaki katika hadhi na usalama katika ardhi ya mtu mwenyewe, unachangia siasa nzuri ambayo inahitajika sana”.

Vile vile Ujumbe huo kwa wasihiriki wa Warsha ya SIGNIS Afrika  anabinisha kuwa Mitiririko ya uhamaji ya nyakati zetu ni usemi wa jambo tata na tofauti ambalo, ili kueleweka vyema, linahitaji uchambuzi wa makini wa kila kipengele cha hatua zake tofauti, kutoka kwa kuondoka hadi kuwasili, ikiwa ni pamoja na uwezekano wa kurudi". Kuhusiana na hilo, Papa Francisko anatualika tujiunge na tukio la kuvutia: “Kuondoa visababishi hivyo na hivyo kukomesha miito ya uhamiaji ya kulazimishwa ya kujitolea kwa pamoja kwa upande wa wote, kwa mujibu wa wajibu wa kila mmoja. Ahadi hii huanza na kuuliza tunachoweza kufanya, lakini pia kile tunachohitaji kuacha kufanya. Tunahitaji kufanya kila juhudi kusitisha mbio za silaha, ukoloni wa kiuchumi, uporaji wa rasilimali za watu wengine na uharibifu wa nyumba yetu ya pamoja.

Tafakari ya pili ni kuhusu jinsi gani. “Ulimi laini utavunja mfupa,” kinasema Kitabu cha Mithali (25:15).  Kwa maana hiyo “Leo kuliko wakati mwingine wowote, kuzungumza kwa moyo ni muhimu ili kukuza utamaduni wa amani mahali ambapo kuna vita; kufungua njia zinazoruhusu mazungumzo na upatanisho mahali ambapo chuki na uadui hukasirika. Katika muktadha wa kushangaza wa mzozo wa kimataifa tunaopitia, ni muhimu kudumisha aina ya mawasiliano ambayo sio ya chuki. Ni muhimu kuondokana na tabia ya kuwadharau na kuwatukana wapinzani tangu awali [badala ya yake ni  kufungua mazungumzo ya heshima”. Kwa hiyo Ujumbe huo unakazia kusema kwamba “Tunahitaji wawasilianaji ambao wako wazi kwa mazungumzo”.

Kama vile Papa Mtakatifu Yohana XXIII alivyohimiza kiunabii katika Waraka wa Pacem in Terris: yaani Amani duniani kwamba  “Amani ya kweli inaweza tu kujengwa katika kuaminiana” (Pace in terries n. 113). Uaminifu kama huo unahitaji jamii shupavu na bunifu ambazo ziko tayari kuhatarisha kutafuta misingi ya pamoja ya kukutana. Inatisha kusikia jinsi maneno ya kuangamiza watu na maeneo yanavyosemwa kwa urahisi. Ndio maana matamshi ya kivita na chuki dhidi ya wageni lazima yakataliwe, pamoja na kila aina ya propaganda inayopotosha ukweli, kuuharibu kwa malengo ya kiitikadi. Kama Wakristo, tunajua kwamba hatima ya amani inaamuliwa kwa uongofu wa mioyo, kwa kuwa virusi vya vita hutoka ndani ya moyo wa mwanadamu. Kutoka moyoni pia huja maneno sahihi ili kuondoa vivuli vya ulimwengu uliofungwa na uliogawanyika na kujenga ustaarabu bora. Juhudi hii hasa inaangukia kwa wawasilianaji wanaotekeleza taaluma yao kama utume

Kama hoja ya tatu,  Kardinali CZerny anawaalika waandishi wa habari kuelewa na kuthamini fursa ambazo wahamiaji hutoa kama njia ya kuleta maisha mapya kwa jumuiya za wenyeji wanao wapokea. Uwepo wao ni fursa nzuri ya kutimiza utume wa uinjilishaji kwa njia ya ushuhuda na mapendo. Kwa kufanya hivyo, waandishi wa habari wa Kikatoliki watakuza ushirikiano wenye ufanisi miongoni mwa vyombo vyote na kumulika kwa hakika  aina mbalimbali (sio usawa) aina mbalimbali za washiriki wa Kikristo kama mali na michango ya wale waliohamishwa kama fursa ya udhihirisho thabiti na unaoonekana wa  Imani yetu ya ukatoliki. Kwa maana hiyo alikazia kuwaalika kuchunguza Mielekeo ya Kichungaji juu ya Huduma ya Wahamiaji wa Kitamaduni na mazoea mazuri ya jumuiya nyingi duniani kote katika juhudi zao za kupanua hema. Kama waandishi wa habari, wao pia ni wakaaji katika hema hilo na wamealikwa kuhamasisha hadi na utu wa watu wote na haki ya kubaki katika ardhi yao wenyewe. Bwana Yesu, Neno aliyefanyika mwili lililomiminwa kutoka moyoni mwa Baba, atusaidie kufanya mawasiliano ya Kikatoliki kuwa wazi, wazi na ya kutoka moyoni.  Katika ujumbe wake wa Mkuu wa Baraza la Kipapa la Huduma ya Maendeleo, alihitimishwa kwa kutoa swali kwao “Je, mimi kama mwandishi wa habari na pamoja na washawishi wengine ninaweza kufanya nini ili watu wetu wawe huru kuchagua kuhama au kubaki?

Ujumbe wa Kardinali Czerny kwa washiriki wa Warsha ya SIGNIS AFRIKA huko Kampala Uganda.
13 July 2023, 15:19