Waziri mkuu wa Belize Mheshimiwa John Briceño Akutana na Papa Francisko Mjini Vatican
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S., Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 20 Aprili 2024 amekutana na kuzungumza na Waziri mkuu wa Belize Mheshimiwa John Briceño, ambaye baadaye amekutana na kufanya mazungumzo na Askofu mkuu Paul Richard Gallagher, Katibu mkuu wa Mambo ya Nchi za Nje, Ushirikiano na Mashirika ya Kimataifa. Katika mazungumzo yao, viongozi hawa wawili wameridhishwa na uhusiano wa kidiplomasia uliopo kati ya nchi ya Belize pamoja na Vatican.
Baadaye viongozi hawa wawili wamejielekeza zaidi kuangalia mchango wa Kanisa katika ustawi, maendeleo na mafao ya watu wa Mungu nchini Belize hususan katika sekta ya elimu na huduma kwa wakimbizi na wahamiaji. Katika mazungumzo yao wamegusia pia masuala mbalimbali ya kisiasa na kijamii nchini Belize kwa kuainisha mchango wa Mama Kanisa katika kutangaza na kushuhudia tunu msingi za maisha ya Kikristo kwa ajili ya ustawi, maendeleo na mafao ya wengi.