2024.10.14 Mhutasari wa Sinodi inayoendelea mjini Vatican 2024.10.14 Mhutasari wa Sinodi inayoendelea mjini Vatican  

Mhutasari wa Sinodi,mchango kuhusu matatizo ya Kanisa na Ulimwengu

Uwazi wa Jumuiya ya kikanisa,kuhusisha watoto,vurugu walizopata watawa ni kati ya mada zilizokabiliwa katika Ukumbi wa Sinodi na kuwakilishwa mhutasari kwa waaandishi wa habari.Waliokuwapo ni Sr Franco Echeverri,rais wa CLAR:usikivu,Askofu mkuu Stankevič,wa Riga:uwajibikaji wa Kanisa na Askofu Sinayobye wa Cyangugu:mchakato wa maridhiano na umoja nchini Rwanda.

Na Tiziana Campisi, Lorena Leonardi  na Angella Rwezaula – Vatican.

Mapendekezo mengi madhubuti yanayotokana na uzoefu tofauti na kushirikishwa kwa uwazi kamili, dhidi ya aina yoyote ya unyanyasaji na kwa wajibu mkubwa wa walei, wanawake na vijana hasa, ndiyo yalikuwa mambo muhimu yaliyojitokeza katika kazi ya Sinodi ambayo bado inaendelea hadi 27 Oktoba 2024 na ambayo imefahamishwa mhutasari wake tarehe 14 Oktoba 2024  katika kikao kifupi cha waandishi wa habari katika Chumba cha Waandishi wa Habari mjini Vatican kilichoanza saa 7.30 mchana na kutambulishwa na naibu Msemaji wa Vyombo vya habari Bi Cristiane Murray. Bi Sheila Pires, katibu wa Tume ya Habari, kwanza  kabisa katika utoaji wa ufupisho wa Sinodi hiyo alichunguza "kazi ya asubuhi ya Jumatatu tarehe 14 Oktoba ya mkutano mkuu wa tisa, uliofanyika mbele ya Baba Mtakatifu Francisko;  pia ule wa Jumamosi asubuhi  tarehe 12 Oktoba na Ijumaa alasiri tarehe 11 Oktoba 2024 kuhusu  masuala yaliyomo katika  sehemu ya njia ya Instrumentum laboris, yaani Kitendea Kazi, kuhusu: “michakato ya kufanya maamuzi, uwazi, uwajibikaji na  tathmini.”

Katika Mkutano huo unaondelea kwa mujibu wa Bi Pires alieleza kuwa  "ilikuwa hasa muhimu sana kusikiliza uzoefu kutoka China, Rasi ya Arabia, Amazonia, visiwa vya Shelisheli na Sahel kuhusu masuala haya".  Na kwa hakika uzoefu huu umeakisi matatizo kama vile, kwa mfano, "ugumu wa kupata maelewano kati ya tamaduni za Kikristo na desturi za mahalia au na kanuni za kiraia kuhusu ndoa.” Hii pia hutokea kwa sababu, ilisemwa katika Ukumbi wa Sinodi kwamba, "Kanisa huko nyuma limepuuza utofauti na ukamilishano kati ya tamaduni.” Wakati huohuo miongozo na mapendekezo yalitolewa kwa msingi wa mambo halisi yaliyopo tayari, kama vile Mkutano wa Kikanisa wa Amazonia ambao, ndani yake, unatoa sauti kwa ukweli tofauti, au uzoefu wa Kanisa la Afrika ambalo linaonesha uhai mkubwa."

Kuwashirikisha watoto katika Kanisa

Katika sehemu mbalimbali, “kulikuwa na mazungumzo mengi kuhusu umuhimu wa kuwashirikisha watoto katika maisha ya Kanisa, sio tu kuzungumzia watoto bali na watoto wenyewe," Bi Pires alibainisha. Hoja zingine zilizooneshwa ni kustawi kwa makatekista, umuhimu wa kuwasikiliza vijana kwa sababu, wakati mwingine, mada na mambo huamuliwa tu  wakati badala yake wanavutiwa na kitu kingine. Zaidi ya hayo, pia kulikuwa na mazungumzo ya kujumuisha shule za Kikatoliki katika mchakato wa uinjilishaji na mafunzo, kwa kuwa zinawakilisha rasilimali muhimu kwa Kanisa. Katika baadhi ya sehemu za dunia, hata hivyo - imeelezwa - Serikali imechukua shule hizi na ajenda ambazo ni kinyume na mafundisho ya Kanisa zinawekwa,” alieleza Bi Pires.

Unyanyasaji wa wanawake watawa

Uingiliaji kati juu ya unyanyasaji wa wanawake watawa, hata katika malezi, ulivutia sana: sio tu unyanyasaji wa kijinsia, bali pia matumizi mabaya ya mamlaka, dhamiri na hali ya kiroho. Imesemekana kuwa wapo wanawake watawa ambao hufanya kazi kwa bidii hasa kuwafikia watu walio katika mazingira magumu zaidi, lakini wanawake wenyewe wanapokabiliwa na masuala yanayohusiana na unyanyasaji wa kingono au unyanyasaji mwingine hushindwa kueleza wasiwasi wao na kutokana na tabia ya mfumo dume wa kijamii hubaki  kimya. Katika suala hilo, ilipendekezwa "kuanzisha taratibu na mifumo katika majimbo na Mabaraza ya Maaskofu ili kushughulikia matatizo haya. Na pendekezo lingine ni kupitia upya sera za kimkataba, ili kuhakikisha hadhi kwa  wanawake waliowekwa wakfu, lakini pia watu wa kawaida kwa ujumla,” Alisisitiza Bi Pires.

Kuna ukosefu wa wanawake na walei waliobobea mafunzo ya Upadre

Bado kuhusu suala la wanawake, katika uingiliaji kati, ilibainika kuwa katika seminari nyingi kuna ukosefu wa uwepo wa wanawake waliowekwa wakfu au walei katika mafunzo ya mapadre, kama vile uwepo wa walei wataalam haupo. Ushiriki wa wanawake, hata hivyo ni msingi kwa sababu wanaweza kuona mambo ambayo wengine hawaoni, wanahakikisha mafunzo ya usawa, wanaboresha mpango wa jumla kwa makuhani wa baadaye,” alihitimisha Bi Peres.

Mashirika ya misaada kwa maaskofu

Katika hotuba yake kwenye mkutano huo huo naye Dk.Paolo Ruffini, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano na rais wa Tume ya Habari, alirejea  juu ya “mandhari ya uwepo mkubwa wa watu wa kawaida na wanawake kwamba nafasi ya kutosha ilitolewa katika makutano haya matatu ya mwisho yenye mada ya michakato ya kufanya maamuzi, ile inayoitwa kufanya mang’amuzi na michakato ya kuchukua maamuzi.”  Katika suala hilo, alisema, "haja ya kuanzisha bodi za watu wa kawaida, wenye mamlaka na wataalam imesisitizwa mara kadhaa, ili kuepusha mizigo mingi kwa wale wanaoshikilia majukumu." Na umuhimu wa kuanzisha mabaraza au kwa vyovyote vile vyombo vinavyoweza kuwa msaada kwa maaskofu au wale wanaoshikilia nyadhifa pia ulisisitizwa. "Kutokana na mtazamo huu, ilisemwa katika baadhi ya hatua iliyoripotiwa na Dk, Ruffini kwamba maamuzi mengi mabaya hapo awali juu ya kesi za unyanyasaji wa watoto katika Kanisa yalichukuliwa na maaskofu ambao labda walikuwa wametengwa au chini ya shinikizo.

Kwa njia hiyo ilipendekezwa kuanzishwa kwa kamati za mashauriano kwa ajili ya Askofu katika majimbo, sio tu kuimarisha ulinzi na kuzuia, lakini pia katika tukio ambalo ni muhimu kurejesha uaminifu wa mapadre walioshtakiwa lakini wakahukumiwa kuwa hawana hatia." Kiukweli, ilisemwa katika Ukumbi kuwa, "kuna upinzani mkubwa wakati mtu anaonekana hana hatia. Lakini kwa msaada wa bodi inayoundwa na wanasaikolojia, wazazi wa watoto walionyanyaswa, wafanyakazi wa kijamii, wasaidizi, itakuwa rahisi kurejesha uaminifu na haki kwa kuhani asiye na hatia."

Uwazi katika Kanisa

Mkuu wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano aliendelea na mrejesho kuwa “Katika hali hiyo hiyo - ilibanishwa kwamba uwazi ni jambo la msingi katika Kanisa la Sinodi, hasa katika nyanja za ulinzi na fedha. Uwazi huu, kama ulivyosisitizwa katika uingiliaji kati ya mwingine, lazima kila wakati usawazishwe na usiri, heshima ya faragha na taarifa nyeti." Aidha Dk. Ruffini aliripoti kuwa wakati wa kazi hizo mada ya uwajibikaji pia ilijadiliwa, ikilenga maana ya kuwajibika: sote tunakubali, ilisemekana, juu ya hitaji la kuwajibika, hata hivyo tulijiuliza ni lazima tuwajibike kwa nani? ulimwengu, kwa maoni ya umma, kwa waandishi wa habari?." Wakati mwingine, kwa hakika, “ajenda zetu za kichungaji na vigezo vya kuwa Kanisa vinaamriwa na matakwa ambayo si yale hasa ya Injili”.

Kwa hiyo kipaumbele ni kuwajibika kwanza kabisa kwa ajili ya Mungu na kwa ajili ya  jamii, ili tusiangukie katika mtego wa kuwajibika kwa matakwa yasiyo ya kiinjili.”  Dk. Ruffini aliongeza kusema kwamba, “ni muhimu kuwajibika kwa Kanisa na si kwa mazingira yoyote ya kibinadamu, kulingana na kanuni za Injili. Sisi si baraza la waelekezi, bali mwili wa fumbo wa Kristo, watu watakatifu wa Mungu.” Na kisha, aliendelea, "kutoa hesabu kwa washiriki walio maskini zaidi, wadhaifu wa Kristo, ambao wanatuhukumu kulingana na jinsi tunavyoishi." Zaidi ya hayo, ilipendekezwa kuimarisha hali halisi ya sinodi iliyopo katika majimbo, parokia, mikutano ya maaskofu" na ilisemekana pia kujifunza kutoka katika Makanisa mapya, kama yale ya Afrika na sio kulazimisha ukweli wa Makanisa ya Magharibi ambayo mara nyingi yako katika articulo mortis. Na kisha pendekezo likaja la kufanya Sinodi za majimbo kuwa za lazima.”

Sinodi katika maisha ya wakfu

Dk. Ruffini vile vile aliripoti kwamba marejeo pia yalifanywa kwa mfano wa maisha yaliyowekwa wakfu ambayo yamekuwa yakijaribu aina za sinodi kwa miaka: juu ya suala hili, utambuzi wa watawa mashuhuda wa Tibhirine ulitajwa ambao waliamua kubaki Algeria katika mazingira ya mateso, vurugu na kutoa maisha yao sio tu sana kwa sababu ya kumtii mkuu wao, lakini baada yake,  kila mmoja kumaliza safari yake ya ndani kwa njia ya sinodi." Zaidi ya hayo, juu ya mada ya uwezekano wa kusasishwa kwa Sheria ya Kanisa, ilisemekana kuwa Kanuni hiyo si chombo cha kushurutisha na cha kusikitisha bali kielelezo cha imani ya Kikatoliki. Kuheshimu sheria ya Kanisa ndiyo njia bora ya kupambana na ukleri na sheria ni ngao inayowalinda waliodhaifu. Pia cha kufurahisha,” alisema Dk. Ruffini, ni kuingilia kati kwa uzoefu wa kichungaji wa Kanisa la Kiafrika ambalo kwa miaka kadhaa limeanza kuandaa makusanyiko ya Dominika bila mapadre, kutokuwepo kwa sababu ya ukubwa wa parokia au umbali kati ya kijiji kimoja na kingine. Haya ni makusanyiko ambamo waamini hukusanyika chini ya wajibu wa makatekista au walei wenye mamlaka kusikiliza neno la Mungu na kupokea Komunio.”

Kuepuka ukleri

Wito wa kuzuia aina yoyote ya ukleri yaani kujiona imerejea tena. Dawa ya kuzuia hilo ilisemwa katika uingiliaji kati ni kuwa na ukaribu kati ya maaskofu  na mapadre, na Mungu na watu wake. Ni uhusiano wenye nguvu na usiotulia, ambao hutatoa ushiriki wa moja kwa moja katika michakato ya kufanya maamuzi. Katika suala hilo, hasa, ilisemekana kwamba hata neno mshauri katika Kanisa linamaanisha jukumu la kusikiliza na kuzingatia. Zaidi ya hayo, katika sehemu  kadhaa ilisisitizwa pia kwamba ni lazima, wakati wa kufanya uamuzi, kueleza sababu zilizowafanya wale walio katika nafasi za uwajibikaji waamue kutenda kinyume na maoni ya kawaida, na kusisitiza nguvu na udhaifu katika kufanya maamuzi na  michakato. Na hasa juu ya hatua hii ya mwisho hasa, katika kuingilia kati, mtindo wa Mtakatifu Cyprian ulikumbukwa aliyesema kwamba: "Hakuna chochote bila jukumu la kibinafsi la askofu, hakuna chochote bila ushauri wa mapadre, hakuna chochote bila idhini ya watu wa Mungu.”

Rwanda kuponya kila mtu

Mauaji ya kimbari ya Rwanda bado si kovu, lakini ni jeraha lililo wazi, kwa maneno ya Askofu Edouard Sinayobye, wa Jimbo Katoliki la Cyangugu, katika jimbo la magharibi mwa Rwanda. “Miaka thelathini ni muda mrefu, lakini inaonekana kama ilitokea jana. Matokeo yake ni mengi na kama Kanisa tunajaribu kuponya watu, iwe ni waathiriwa au wahalifu. Tunajifunza kuwa kaka na dada.” Kwa njia hiyo akizungumza katika muhtasari uliofanyika katika Chumba cha Waandishi wa Habari cha Vatican, kiongozi huyo alieleza jinsi ambavyo Kanisa linavyoandamana na jaribio gumu la kuzaliwa upya, na nini maana ya uzoefu wa sinodi kwa Rwanda. Kama  tunavyosoma katika kitabu cha Matendo ya Mitume Askofu Sinayobye alisema: “Kama vile wanafunzi , walikuwa moyo mmoja karibu na Petro na Maria, tunapitia sinodi karibu na Papa Francisko, ambayo ni ishara na karama ya umoja wa Kanisa na ni katika mchakato huu wa sinodi ndipo njia ya upatanisho na umoja ipo.”

Kukebisha kitambaa kilichoraruliwa na mauaji ya kimbari

Wakati, kama mkutano wa maaskofu, ulipata  ukaribu wa kwanza kwa Sinodi mchakato ulikaribishwa kama kairòs, kwa sababu ushirika ni dhana fasaha katika kitovu cha Rwanda: Sinodi ina uzoefu kama fundisho linalotupatia misingi ya kibiblia na ya kitaalimungu kuelewa kwamba sisi ni kitu kimoja. Kuzungumza kuhusu udugu kunatusaidia kuelewa kwamba sisi ni kaka na dada,” alisisitiza Askofu wa Cyangugu. Sinodi kwa hiyo inakuwa mtindo wa maisha ya kiroho ambayo inakumbusha “namna ya kuishi na kutenda kwa Kanisa, na  kwa   wote. Katika awamu ya usikilizaji, alikumbusha kwamba, “katika kila jimbo tulikutana na kila mtu, kuanzia jumuiya za kikanisa hadi watoto, kupitia watu waliowekwa wakfu na watu walio pembezoni, wafungwa, makahaba, walemavu na kuanzisha mafunzo ya kimisionari ambayo yanahusu kila mtu, hasa watu wa kawaida: kwa hivyo Sinodi husaidia kuimarisha huduma za kichungaji, ambazo ni mahali pa kuanzia kwa ajili ya kurekebisha hali ya kibinadamu na kijamii iliyosambaratishwa na mauaji ya kimbari.”

Mada za michakato ya Sinodi

Mtaalimungu, Sista Gloria Liliana Franco Echeverri, ambaye pia alishiriki katika Sinodi ya Amazonia(2019) na ni rais wa Shirikisho Baraza la Watawa wa Amerika Kusini (CLAR) alisema: “Tulitambua, katika muhtasari, kwamba mafunzo yana mantiki tu, ikiwa tunayafanya kama mashuhuda, ikiwa ni muhimu na yanaanzia msingi wa kianthropolojia, unaojumuisha na kuzingatia ukweli; utambuzi ni ufunguo wa kujibu katika ngazi ya eneo, unatupatia uwezekano wa kuelewa kile ambacho Roho antuomba  kwa kuwa ukweli wa Kanisa ni tofauti, unapata nyakati tofauti na vipaumbele.” Zaidi ya hayo, mtawa huyo aliendelea, katika mijadala ya siku chache zilizopita kuhusu umuhimu wa miundo shirikishi ambayo umejitokeza, pamoja na thamani ya uwazi kama utamaduni badala ya njia, yenye uwezo wa kupenyeza taratibu za utambulisho wa Kanisa.”

Kujifunza na kushirikisha

Askofu Zbignevs Stankevičs, mkuu wa Riga, Nchini Latvia alisisitizia juu ya lengo la mwisho  la "utume" kwamba “ikiwa Sinodi inalenga kuachilia zawadi na karama za kila mtu aliyebatizwa, maaskofu, mapadre wa parokia na viongozi wa vikundi mbali mbali hufanya kazi kulingana na jukumu la pamoja kueleweka kwa maana ya kiroho. Pia, akirejea uzoefu wake mwenyewe kama maaskofu nchini Latvia, hasa kushiriki matendo mema ya kichungaji kama chanzo cha msukumo kwa wachungaji, makamu wa rais wa Baraza la Maaskofu wa  Latvia kwa njia hiyo  alitaja kustawi, katika miaka ya hivi karibuni, kwa shule za uinjilishaji na, kwa ujumla, ya mipango inayowasha moto wa uinjilishaji.  Hatimaye,Askofu Mkuu  Stankevičs alizungumza kuhusu "Ukarabati wa kimungu na  uzoefu wa kufufua parokia zilizozaliwa Canada, ambapo huduma 80 na watu wa kujitolea 800 waliojishughulisha na shughuli zilifanikiwa katika jumuiya ambayo ilikuwa karibu kutoweka. "Ninaamini  kwamba tunahitaji kuangalia mahali ambapo Roho wa Mungu anatenda na kujifunza, kushiriki. Sio tu wakati wa Sinodi, lakini pia baadaye. Alihitimishwa

Umuhimu wa kusikiliza

Katika nafasi iliyojitolea kwa maswali ya waandishi wa habari, aliyekuwa wa  kwanza kuulizwa alikuwa Sr  Gloria Liliana Franco Echeverri, wa Shirika la Wasindikizaji wa Mama Yetu Maria ambaye aliulizwa ikiwa alisikiliza kipengele ambacho mkazo malum uliwekwa katika Sinodi hii juu ya sinodi, ambayo leo hii ni msukumo unaozidi kupitishwa katika Amerika ya Kusini na kwingineko. Mtawa huyo alisisitiza kwamba kwa hakika sinodi hii, iliyodumu  kwa miaka miwili, iliyotangulia, mnamo 2018, juu ya Vijana, imani na utambuzi wa ufundi, na pia ile ya Amazonia, mnamo 2019, imeakisi umuhimu wa 'kusikiliza kama mchakato wa ubinadamu. Kwa Sr  Franco Echeverri, uzoefu wa sinodi uliishi kama maabara ambao unaturuhusu kubadilisha njia ya kuwasikiliza wengine, kwa sababu kuna mengi ya kujifunza katika jamii, kusikiliza kunatoa uwezekano wa kuyafikia mapenzi ya Mungu kwa njia ya heshima zaidi. "Tuko katika mchakato huu wa kujifunza," aliongeza, akielezea kwamba kusikiliza kunajitokeza kama shughuli muhimu katika Kanisa.

Shemasi wa kike

Mada ya shemasi wa kike ikaguswa tena na Askofu  Sinayobye aliyeulizwa kutoa  maoni yake binafsi maana yeke. Kwa mara ya kwanza Askofu huyo alieleza kwamba “barani Afrika hakuna huduma ya Ushemasi ya kudumu, bali ni jukwaa tu la ushemasi katika njia ya kuelekea ukuhani.” Kuhusu uwezekano wa mashemasi wanawake, Askofu wa Cyangugu alisema “ni suala ambalo bado iko kwenye mafunzo  kwa umakini mkubwa, kwa kuzingatia nuru iliyotolewa na  Majisterio ya Kanisa. Kuhusu maoni yake mwenyewe, Askofu  Sinayobye alifafanua kwamba, kama Askofu, yuko katika ushirika kamili na maaskofu wengine na zaidi ya yote na Papa na kwa hivyo hana shida yoyote ikiwa shemasi wa kike atakubaliwa kwa sababu “si suala la hisia, sisi ni wachungaji wa watu wa Mungu, walinzi wa imani, hisia zetu na usikivu wetu havihesabiki, haviwi mbele, na tuko katika ushirika.”

Utamaduni wa utunzaji

Kuhusu mada ya udhalilishaji wa wanawake watawa iliyoibuka katika Kikao tarehe 14 Oktoba ukumbini wa Sinofi,  swali liliulizwa iwapo uelewa mkubwa kuhusiana na tatizo hilo unaweza kujitokeza katika Sinodi hii.Bi Sheila Pires alibainisha kuwa suala hilo linachambuliwa na kutathminiwa iwapo litajumuishwa katika hati ya mwisho, huku Sr  Franco Echeverri alizingatia hitaji la utamaduni wa kujali,kwa  kubainisha kwamba kazi kubwa inafanywa juu ya mahusiano ndani ya Kanisa, kwa mapitio ya mitazamo hiyo ambayo haiendani na mtindo wa Yesu. Kwa wanawake waliowekwa wakfu, maisha ya wanawake watawa hayapaswi kubaki pembeni na mchakato huu wa sinodi unaturuhusu kuzingatia chaguo la utamaduni wa utunzaji.” Askofu  Stankevič, kwa upande wake, alisisitiza kwamba tatizo la unyanyasaji wa wanawake watawa linahusu sinodi hiyo, kwa sababu “ni kikwazo kwa utume wa Kanisa, kwa vile inaumiza watu, kwa hiyo ni lazima ishughulikiwe.”

Matunda ya mchakato wa sinodi

Hatimaye Askofu wa Cyangugu alipoulizwa jinsi mchakato wa sinodi ulivyopokelewa nchini Rwanda alifafanua kuwa, Kanisa limetoa mwaliko kwa kila mtu kusafiri pamoja na kwamba ujumbe huu unawakilisha mchango mkubwa katika upatanisho nchini humo. Mapadre, watu waliowekwa wakfu na walei walikutana na watu wengi, walikwenda shule, magereza, ambako kuna wafungwa wengi wanaotuhumiwa kwa uhalifu wa mauaji ya kimbari; kuzungumza na watu hawa kuhusu msamaha ni fursa ambayo njia hii ya sinodi inatoa, pia kutokana na misingi ya Biblia ambayo Sinodi inatoa kwa ajili ya umoja na upatanisho,”alihitimisha Askofu  Sinayobye wa Jimbo la Cyangugu, Rwanda.

14 October 2024, 18:00