Muhtasari wa Sinodi-Siku ya 13:Mkutano wa Mediterania kusikiliza wahamiaji

Katika mkutano na waandishi wa habari tarehe 17 Oktoba,katika Ofisi ya Vyombo vya Habari vya Vatican,sifa zilitolewa kwa ajili ya kazi ya Makanisa yanayojitolea kutunza uchungaji kwa ajili ya uhamaji wa binadamu.Msisitizo pia uko kwenye umakini kwa vijana na watu wenye ulemavu,huku kukiwa na wito wa kuwa na uhusiano thabiti kati Curia Romana na Jumuiya za watu wa Asili.

Na Antonella Palermo,Roberto Paglialonga na Angella Rwezaula–Vatican.

Wakati wa kikao cha asubuhi cha Sinodi tarehe 17 Oktoba 2024 wazo la "kusanyiko la Kanisa la Mediterranea lilipendekezwa ili kusikia sauti za wahamiaji. Mkutano huo ulitoa shukrani kwa nafasi ya Makanisa katika kuwakaribisha wahamiaji na kusifu mitandao inayounga mkono utume huu. Miongoni mwa mada zilizojadiliwa ni umakini uliotolewa kwa vijana na kwa wale walio na ulemavu, kwa matumaini ya uhusiano mkubwa kati ya Curia Romana na Jumuiya za Watu wa Asili. Na iliripotiwa kuwa tarehe 18 Oktoba Makadinali Hollerich na Grech, Sr  Salazar, na Askofu Flores watakutana na wanafunzi wa chuo kikuu kujadili mada kutoka katika Sinodi inayoendelea.

Kuzingatia ulemavu na mazungumzo ya dini tofauti

Washiriki 346 walikuwepo kwenye Ukumbi, wa Paulo VI na majadiliano yaliendelea na uingiliaji kati kuhusu  mada 2 na 3 ya Instrumentum Laboris(kitendea kazi). Kulikuwa na wito wa kuhuisha jukumu la parokia, ushirikishwaji wa moja kwa moja wa vijana, na umakini wa kweli kwa watu wenye ulemavu, ikiwa ni pamoja na kuundwa kwa baraza maalum kwa ajili yao. Masuala mengine yaliyotolewa ni pamoja na jukumu la "mitandao ya kimitandao," kama vile Talitha Kum, na jinsi ya kuiunganisha katika Mabaraza ya Maaskofu, pamoja na pendekezo la jukwaa la pamoja kwa wanafunzi tofauti wanaohudhuria shule za Kikatoliki.

Uhusiano wenye nguvu kati ya Roma na Makanisa mahalia

Dk Paolo Ruffini, Mwenyekiti  wa Baraza la Kipapa la  Mawasiliano, aliakisi jukumu muhimu la mashirika ya kitawa, hasa katika maeneo yenye mateso makubwa na dhiki au elimu. Pia alisisitiza umuhimu wa kuimarisha uhusiano kati ya sinodi na ukuu ambao umejadiliwa katika vikao vya wazi. Dk. Ruffini alidokeza kwamba, inashangaza kwamba, miaka mingi sana baada ya Mtaguso wa Vatican II, hali ya kitaalimungu ya Mabaraza ya Maaskofu bado haijafahamika. Pendekezo hilo lilitolewa ili kushauriana na Makanisa mahalia zaidi wakati wa kuandaa hati na kwa ajili ya Baraza la Kipapa husika ili kutembelea jumuiya ndogo na majimbo mara nyingi zaidi.

Kujenga vifungo vya kidugu

Sr. Samuela Maria Rigon, Mkuu wa Shirika la  Masista wa Mama mwenye Huzuni, alizungumza kuhusu uzoefu wa sinodi na kusisitiza umuhimu wa kujenga uhusiano wa kidugu. Alibainisha kuwa karibu robo ya washiriki wa Sinodi ni watu wa kawaida, vijana, na watawa, ambao wote wana fursa ya kuzungumza. Ingawa mivutano inatokea kutokana na mitazamo tofauti kuhusu mada fulani, alieleza kuwa haya si ubaguzi na wala itikadi nyingi bali ni kama vile mienendo ya kawaidia ya kiume/kike.

Sinodi katika Kanisa la Asia

Kardinali Charles Bo, Askofu Mkuu wa Yangon, na Myanmar, na Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Asia (FABC), alitoa maelezo mafupi ya mchakato wa sinodi barani Asia. Alizungumza kuhusu kuongezeka kwa ushiriki wa vijana katika uinjilishaji wa kidijitali, mipango bunifu ya kichungaji, na changamoto zinazoletwa na ukleri. Licha ya upinzani kutoka katika baadhi ya maaskofu, FABC imeridhishwa na hatua iliyofikiwa, hasa kujitolea kwa Kanisa kusikiliza kila mtu.

Haja ya mabadiliko ya muundo

Kardinali Gérald Cyprien Lacroix wa Québec, Canada, alisisitiza umuhimu wa Kanisa “kusikiliza,” hasa wale walio tofauti na kuepuka kutatua matatizo kwa njia ya vurugu pekee. Alitoa wito wa mabadiliko ya kimuundo, hasa katika mazoea ya utume, vyombo vya habari, na kuimarisha maisha ya kiroho.

Kuzoea ulimwengu wa kisasa

Mazungumzo hayo pia yaligusia ufafanuzi kati ya Mabaraza ya Roma na Maaskofu, na uhusiano kati ya kusikiliza na kutekeleza mabadiliko. Dk. Ruffini alieleza kwamba wazo la kutoa mamlaka zaidi kwa Makanisa mahalia limekuwa tafakari ya muda mrefu ndani ya Kanisa, hasa tangu Mtaguso wa Vatican II.

Uwezekano wa Baraza la kusikiliza

Pendekezo la "baraza la kusikiliza" lilitolewa lakini bado linajadiliwa ambapo Kardinali Bo alisisitiza kwamba Sinodi hii ni ya kipekee kwa sababu kweli ni mchakato, na anatumaini kwamba kila Askofu atafikiria kufanya sinodi ya jimbo ili kuendeleza kazi iliyoanza hapa.”

17 October 2024, 17:18