2024.10.19 Mazungumzo na wanafunzi wa Vyuo vikuu kuhusu Sinodi. 2024.10.19 Mazungumzo na wanafunzi wa Vyuo vikuu kuhusu Sinodi. 

Viongozi wa Sinodi wamejibu maswali ya wanafunzi wa vyuo vikuu

Viongozi wa Sinodi wameshughulikia maswali yenye changamoto kutoka kwa wanafunzi wa vyuo vikuu ambao ni wanafunzi kutoka sehemu mbali mbali za Marekani waliokutana mjini Roma ili kufanya mazungumzo na uongozi wa Sekretarieti ya Sinodi.

Na Linda Bordoni na Angella Rwezaula -Vatican.

Wanafunzi wa Vyuo Vikuu wapatao 140, hasa kutoka Amerika Kaskazini, walikusanyika katika Ukumbi wa Paulo VI, Ijumaa jioni tarehe 18 Oktoba 2024 ili kushiriki moja kwa moja na viongozi wa Sekretarieti ya Sinodi. Tukio hilo lililopewa mada ya: “Wanafunzi wa Vyuo Vikuu katika Majadiliano na Viongozi wa Sinodi,” lilijumuisha msururu wa maswali muhimu yaliyoulizwa na wanafunzi na kujibiwa na Kardinali Mario Grech, Katibu Mkuu wa Sinodi, Kardinali Jean-Claude Hollerich, Mjumbe wa Sinodi, Sr. Leticia Salazar, Chansela wa Jimbo la Mtakatifu  Bernardino, na Askofu Daniel Flores wa Jimbo la  Brownsville kusini mwa Texas. Mpangilio wa mkutano huo kwa  pande zote, ulioakisi ule wa Kikao cha 2 kinachoendelea cha Sinodi ya Kisinodi, unaashiria maono ya Papa Francisko kwa Kanisa kutembea pamoja katika safari ya kusikiliza na kujihusisha.

Kushughulikia changamoto ya kusikiliza

Swali la kwanza lilitoka kwa Asia Chan, mwanafunzi kutoka Trinidad na Tobago, ambaye alionyesha ugumu wake kueleza imani yake katika utamaduni tofauti na kuuliza jinsi Kanisa lingeweza kuboresha mashauriano ya siku zijazo ili kuhakikisha sauti zaidi zinasikika. Kardinali Grech alijibu, akikubali changamoto na kushirikisha kwamba mchakato wa sasa wa sinodi ya Kanisa kwamba hauna kifani katika mtazamo wake wa kusikiliza. Alibainisha kuwa ingawa bado kuna nafasi ya kuboreshwa, sinodi hii imehusisha watu wengi zaidi kuliko waliotangulia. "Wakati wa Sinodi ya Familia" Kardinali alisema, "Mikutano 80 kati ya 114 ya Maaskofu tu  ndiyo iliyoshirikishwa. Wakati huu 112 kati ya 114 waliwasilisha ripoti yao: hiyo inamaanisha kuwa watu wengi wamesikilizwa. Pia alibainisha kuwa wakati huu zaidi ya watu 20,000 walishiriki kwenye jukwaa la kidijitali, hivyo "Ushiriki umekuwa mzuri sana na unaahidi kuwa bora zaidi katika siku zijazo.” “Kusikiliza ni jambo la msingi,” aliendelea, akisisitiza umuhimu wa kusikiliza kwamba sio maoni tu bali pia mwongozo wa Roho Mtakatifu katika mchakato ambao “utasaidia Kanisa kuwa sinodi zaidi, na kujenga utamaduni wa kukutana unaojikita katika kumsikiliza Mungu na kila mmoja wao.”

Kushirikisha vijana walioko pembezoni

Alexandra, mwanafunzi wa Venezuela ambaye alikulia Mashariki ya Kati, aliuliza kwa nini vijana wasiojihusisha na Kanisa wanapaswa kujali kuhusu sinodi, na jinsi gani  Kanisa linavyoweza kuunda nafasi kwa wale wanaohisi kuumizwa nalo. Kardinali Hollerich alisisitiza umuhimu wa kuwasikiliza watu, si maoni yao tu, katika ulimwengu wa kisasa wenye mgawanyiko. Aliashiria mgongano wa maoni ambayo kwa sasa ni sifa ya Marekani na kusema "Mwelekeo kuelekea kituo cha kipekee ni njia ya kufikiri mbali sana na sinodi, kama ilivyo ulimwengu wa digitali, ambapo unafuata watu tu ambao wana maoni sawa na wao na ikiwa hukubaliani inakuwa upinzani sana.” Lakini, aliongeza, “Mtu mwenye maoni tofauti si adui; sisi ni sehemu ya ubinadamu sawa. Lazima tutafute masuluhisho ya pamoja.” Katika Kanisa, alisema, ni rahisi zaidi kwa sababu sisi ni dada na kaka; tunashiriki Ubatizo huo huo. "Nadhani ulimwengu unaweza kujifunza kutokana na hilo na itakuwa vyema ikiwa tunaweza kufungua imani na dini nyingine ili kujadili katika udugu wa kimataifa masuala makubwa ya ulimwengu wetu kama sinodi hutoa njia ya kuleta watu pamoja, wakitambua ubinadamu wao wa pamoja.” Na “Ulimwengu unaweza kujifunza kutoka kwa mtazamo wa Kanisa kwa sinodi, hasa katika kuunda nafasi za mazungumzo ya heshima ambayo yanashughulikia masuala ya kimataifa kama vile amani, haki na ikolojia,” Kardinali Hollerich alisema.

Uaminifu kwa utamaduni huku kukiwa na mabadiliko ya sinodi

Sondra, mwanafunzi kutoka MMtakatifu Francisco, aliibua wasiwasi kuhusu jinsi mkazo wa uzoefu katika mchakato wa sinodi unaweza kuathiri uaminifu wa mapokeo na ukweli. Askofu Flores alijibu kwa kumhakikishia kwamba sinodi haiathiri utume wa Kanisa wa kutangaza Injili. Alikiri changamoto ya kuwasikiliza wenye mitazamo tofauti lakini akasisitiza kuwa ni muhimu kuelewa hali halisi ya watu. "Unabakije mwaminifu kwa Kanisa? Kanisa limekuwa na fujo kwa miaka 2000, lakini Roho analiweka pamoja. Nitaleta nini Roma kutoka Kusini mwa Texas? Sina wasiwasi kwamba imani ya Kanisa itaathiriwa tunasikilizana,” alisema. Mchakato wa sinodi, alieleza husaidia kuongeza uelewa bila kudhoofisha mafundisho ya msingi ya Kanisa.

Kuhama kutoka katika majadiliano kwenda katika vitendo

Joseph, mwanafunzi kutoka New Orleans aliyehusika katika huduma ya vijana, aliuliza jinsi gani sinodi inaweza kubadilisha mijadala kuwa hatua madhubuti. Sr. Leticia Salazar alisisitiza hali ya mabadiliko ya mchakato wa sinodi. Aliufananisha na mwaliko wa Mtakatifu Ignatius wa Loyola kujionea maandiko kana kwamba mmoja alikuwapo kwenye eneo la tukio. Kuketi kwenye meza sawa na washiriki wa sinodi, alisema, ni uzoefu wa nguvu unaokuza ushirika na mabadiliko. Sr Leticia alionyesha matumaini kwamba wanafunzi wangerudisha uzoefu huu kwenye jumuiya zao, na kufanya sinodi kuwa ukweli halisi. Aliongeza kuwa mchakato huo si wa kinadharia tu bali ni njia ya kupambanua na kujenga pamoja kama Kanisa moja. “Nini kitaendelea baada ya muda huu hapa? Itaendelea Mtakatifu Bernardino na kwa matumaini katika Kanisa zima,” alisema. "Ni njia ya kumpata Yesu kati ya mtu na mwingine, sio wazo, ni kujenga pamoja na kutambua pamoja mapenzi ya Mungu." Katika wakati huu wa mgawanyiko, Sr Leticia aliendelea, "Sinodi ina njia ya upole ya kutangaza Habari Njema kwa njia ya heshima sana.  Nina matumaini makubwa kwa Marekani kuwaona hapa,” alimalizia, ni kwamba  “Uzuri hatuko peke yetu. Papa Francisko hataki kufanya utume wake mwenyewe; aliita Kanisa zima kufanya hivyo pamoja naye. Ufanywe kweli!”

Sinodi katika malezi ya kiteolojia na kihuduma

Fabio kutoka El Salvador, msomi wa taalimungu, aliuliza jinsi gani seminari na shule za taalimungu  zingeweza kukuza sinodi. Askofu Flores alijibu kwa kuwahimiza wataalimungu na waseminari kujihusisha na hali halisi ya watu wanaowahudumia. Alisisitiza umuhimu wa kutoka nje ya mazingira ya kitaaluma ili kupata uzoefu wa maisha ya wale walioko pembezoni. Kardinali Grech aliongeza kuwa seminari na programu za taalimungu lazima zitathminiwe upya kupitia lenzi ya sinodi. Aliwaalika wanafunzi na wataalimungu kuchangia katika mazungumzo haya yanayoendelea, akisisitiza kwamba sinodi lazima ipenye kila ngazi ya malezi ya Kanisa.

Mazungumzo ya dini mbalimbali na sinodi ya kimataifa

Mika kutoka Cincinnati aliuliza swali la 6 na la mwisho kuhusu jinsi gani Kanisa linavyoweza kuunga mkono walei katika kukuza mazungumzo ya dini mbalimbali na mafunzo gani sinodi inaweza kujifunza kutoka kwa mapokeo mengine ya imani. Kardinali Hollerich alitafakari kuhusu uzoefu wake huko Japan, ambako alifundisha wanafunzi wa dini mbalimbali. Alishirikisha jinsi gani mkutano huo ulimsaidia kutambua kwamba Mungu yuko tayari katika tamaduni na dini zote. Kardinali alisisitiza kwamba, sinodi inaweza kufundisha walimwengu kwamba, dini isiwe chanzo cha migogoro, bali ni njia ya kuelekea udugu mkubwa zaidi, na kulitaka Kanisa kufanya kazi pamoja na mapokeo mengine ya kiimani ili kutatua changamoto za kimataifa, kama vile haki ya kijamii na ikolojia. kaka na dada waliounganishwa na misheni ya pamoja. "Lazima tuoneshe , si atu, tunapaswa kuchukua hatua pamoja, kukutana pamoja na kukua kwa heshima, upendo na urafiki na kuchukua hatua kwa manufaa ya ubinadamu. Hiyo ni sehemu ya utume wetu, na sehemu ya utume huo pia ni kumtangaza Mungu,” alisema.

Mkusanyiko wa maombi na maswali

Mwishoni mwa kipindi, wanafunzi waliwasilisha mchoro wa (mosaic) unaowakilisha sala na maswali ambayo yalikuwa yametokea wakati walipokuwa Roma. Kila mmoja wa wanajopo alialikwa kuchangia maombi, kuashiria tumaini la pamoja la Kanisa la Sinodi, shirikishi na linalosikiliza zaidi.

19 October 2024, 11:22